KWELI umaskini mbaya. Baraza la Soka la Afrika Mashariki na Kati
(Cecafa) limeitamani timu ya soka ya Ivory Coast ije katika mashindano
yake ya Challenge Cup, lakini limezichungulia gharama za kukileta kikosi
hicho cha kina Didier Drogba, likaona maji mazito na limetamka:
“Hatuwezi kumleta Drogba.”

Katibu Mkuu wa Cecafa, Nicholas Musonye, amesema
kuisafirisha timu hiyo hadi mjini Nairobi itagharimu Dola 25,000 (Sh2.1
milioni) na kwamba hadi sasa baraza hilo halijakuwa na uhakika wa kupata
mdhamini wa mashindano hayo. “Ninapenda kutangaza kwamba tumefuta
mpango wa kuialika Ivory
Coast kwenye mashindano yetu. Tatizo ni gharama
kubwa za kikosi chao.Hatuwezi kutumia zaidi ya Dola 25,000 kwa ajili ya
timu moja tu, gharama zao ni kubwa na hatuna uhakika wa fedha,” alisema.

Hata hivyo, Musonye, alisema sasa Zambia na Malawi zimeshathibitisha kushiriki.
Licha ya kuifuta Ivory Coast, Musonye, pia ametoa
wito kwa kampuni na mashirika kujitokeza kudhamini mechi
za mashindano hayo.
“Tuna tatizo hapa, tumejaribu kuwasiliana na
mashirika na kampuni kadhaa za taifa hili lakini hadi sasa hakuna
mafanikio yoyote,” alisema.
“Mwaka jana tulipoandaa mashindano haya Somalia,
kampuni za Kenya ndizo zililalamika kwamba tungeyaleta mashindano hapa.
Sasa tumewaletea hatuwaoni, kampuni za Kenya zipo wapi?” Alihoji
Musonye.
Mashindano hayo ambayo yalizinduliwa mwaka wa 1926, yatahudhuriwa na Rais wa Shirikisho la Soka la Afrika (CAF), Issa Hayatou.
0 comments:
Toa Maoni yako
Tuambie Unafikilia Nini..!